Kuna mambo mengi madogo madogo lakini ya MUHIMU katika
kutimiza mambo yako ya kila siku, mambo hayo wengi hawayatilii maanani aidha
kwakuwa hawajui umuhimu wake au wanayapuuza. Mimi huwa namfananisha mtu mwenye
ndoto au malengo kama DEREVA na ndoto yake au malengo yake ni kama MZIGO ambao
inabidi aufikishe sehemu husika. Kila Dereva huwa anatamani awahi kufika
anakoelekea ili apate mshahara wake, shauku ya zawadi au mshahara wake ndiyo
inayomfanya afanye juhudi kwa nguvu na ujuzi alionao ili afikishe mzigo kwa
wakati mwafaka. Lakini njiani anazingatia alama mbalimbali za barabarani
zinazomuongoza afike salama.
Hata katika maisha yetu kuna mambo mbalimbali tunayotakiwa
tuyatumie ili kufika salama na pia kwa wakati, mambo haya yanatupa tahadhari
juu ya yaliyo mbele yetu.
Je, katika mipango yako ya maisha iwe biashara, kilimo,
Elimu, Sanaa yako huwa unahusisha na taarifa za utabiri wa mamlaka za sekta
husika. Wewe ni mkulima je unafuatilia matangazo na tahadhari zinazotolewa na
mamlaka ya hali ya hewa pamoja na idara ya masoko?. Je wewe mfanya biashara
mara unafuatilia mabadiliko ya bei na taarifa nyingine muhimu kutoka mamlaka ya
masoko? Je wewe mwanafunzi hiyo kazi unayosomea miaka kadhaa ijayo hali ya
ajira itakuwaje?
Watu wengi huwa hawaoni umuhimu wa mambo haya lakini kwa mtu
ambae uneapanga mipango yako vizuri na kwa ustadi lazima uzingatie mambo haya
ambayo yatakufanya upange njia mbadala ikiwa mambo yatabadilika tofauti na
ilivyotegemewa. Mkulima ili ufanikiwe lazime ulime mazao yanayoendana na
taarifa za kiasi cha mvua kinachotegemewa kwa mwaka huo. Vile vile mfanya
biashara lazima ujue bidhaa gani inayoendana na hali ya hewa inayotarajiwa
ndani ya mwezi au wiki ijayo.
Lakini taarifa hizi pia zinaweza kutumika kwaajili ya
mipango ya mda mfupi, au ratiba yako ya kila siku. Unapanga safari lakini je
umefuatilia hali ya hewa kesho itakuwaje ili ujiandae vizuri, au una mpango wa
kumtembelea rafiki yako mshauriane kuhusu maisha je, unaangalia hali ya hewa ya
kesho itakuwaje au unasubiri uahirishe ratiba yako baada ya kushuhudia hali ya
hewa mbaya? Wengi hupuuza mambo haya na kuchukulia kuwa ni mambo yasiyo na
umuhimu. Unapopanga kupeleka bidhaa yako sokoni au eneo lililo mbali na eneo
lako je unafuatilia bei elekezi za bidhaa hiyo kule unakopeleka.
Kama unahitaji kufanikisha mipango yako basi lazima ujiandae
kukabiliana na kuendana na hali halisi ya kesho, panga ratiba yako vizuri ili
usiwe mtu wa kuahirisha mambo. Tumia vyombo vya habari kama vile magazeti,
redio, televisheni n.k kupata habari na matukio yanayotarajiwa katika sekta
uliyoilenga wewe.
KUMBUKA: Mafanikio yako yanachangiwa na mambo madogo madogo unayoyafanya kila siku, hivyo kila jambo lichukulie uzito wake.
KUMBUKA: Mafanikio yako yanachangiwa na mambo madogo madogo unayoyafanya kila siku, hivyo kila jambo lichukulie uzito wake.



Comments
Post a Comment